Nyon, Uswisi. Shirikisho la Soka Ulaya (Uefa) limeizuia klabu ya soka ya Barcelona kusajili wachezaji wapya kwa miezi 12.
Adhabu hiyo ambayo inakwenda sanjari na faini ya
Euro 306,000 inatokana na Barcelona kukiuka kanuni kwa kusajili makinda
wenye umri chini ya miaka 18 kutoka sehemu mbalimbali nje ya Hispania na
kuwaweka katika shule yake ya soka, La Masia.
Pia, Shirikisho la Soka la Hispania limetozwa Euro 340,000 kwa kosa hilo, Fifa imeeleza jana.
Fifa imesema Barcelona imekuwa ikishawishi vijana wenye umri wa kwenda shule na kuwasajili kupitia mfumo wake wa kukuza vipaji.
Adhabu hiyo kubwa imewahi kuikumba Chelsea msimu wa 2009 baada ya kumsajili kinda wa klabu a Lens ya Ufaransa, Gael Kakuta.
Hata hivyo, adhabu hiyo ilifutwa baada ya klabu hiyo kukubaliana na Lens na kulipa Euro 3 milioni.
Shirikisho hilo la soka limeeleza kuwa kwa muda mrefu Barcelona imekuwa ikirubuni makinda hao, jambo ambalo halikubaliki.
Kanuni za Fifa zinataka sheria za kimataifa za
uhamisho wa wachezaji zifuatwe na kuzingatiwa kwa wachezaji wenye miaka
18, isipokuwa kwa matukio maalumu na kwa ruhusa ya Kamati ya Hadhi ya
Wachezaji.
Kamati ya Nidhamu ya Fifa imesisitiza haja ya
kuwalinda wachezaji chipukizi na kuzingatiwa kwa kanuni za usajili na
uhamisho wa wachezaji kimataifa.
0 comments: