Ofisi ya Rais (Ikulu) imesema haikuwatupia virago wajumbe wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu ilitoa
taarifa hiyo jana ikirejea taarifa zilizomnukuu aliyekuwa Mwenyekiti wa
Tume hiyo, Jaji Joseph Warioba akisema: “Ikulu imetutupia virago.”
Jaji Warioba alikaririwa akilalamikia jinsi yeye
na makamishna wa tume, walivyoondolewa ofisini na kunyang’anywa magari
kwa haraka bila kusubiri siku waliyokuwa wamepanga kufanya makabidhiano.
Taarifa ya Ikulu ilisema kifungu cha 31 (1) cha
Sheria ya Mabadiliko ya Katiba kinasema shughuli za tume zinakoma baada
ya Mwenyekiti wake kuwasilisha Rasimu ya Katiba kwenye Bunge Maalumu la
Katiba.
Ilifafanua kuwa Jaji Warioba aliwasilisha Rasimu
ya Katiba bungeni Machi 18, 2014 na siku iliyofuata Machi 19, 2014 na
kwa mujibu wa Sheria Rais alitia saini tangazo la Serikali kuvunja tume
hiyo.
Ilisema tangu mwanzo wajumbe, mwenyekiti,
Sekretarieti ya Tume na Watanzania wote waliijua siku ya mwisho ya Tume
kukamilisha shughuli zake, hivyo kwa mtu “kujitia ameisahau siku hiyo ni
kiwango cha juu sana cha unafiki.”
“Siku hiyo ya mwisho iliwekwa kwa mujibu wa Sheria
ya Mabadiliko ya Katiba, na Ikulu haikuwa na madaraka wala mamlaka
yoyote kubadilisha tarehe hiyo.
Hivyo, madai ya Ikulu kuitupia virago Tume ya
Mabadiliko ya Katiba hayana msingi wowote na ni jambo la kutunga tu,”
ilisema taarifa hiyo.
Ilisema tangu Tume ilipovunjwa, haikuwa tena na kazi ya kuandaa ripoti au Rasimu kwa sababu kazi hiyo ilikuwa imekwisha.
Kuhusu muda wa kuandika ripoti ya makabidhiano,
taarifa hiyo ilihoji kuwa tangu Desemba 30, mwaka jana sekretariati
ilikuwa na muda wa siku 77, ilishindwa nini kuiandaa wakati maofisa wake
walikuwa wanaendelea kulipwa mshahara na Serikali.
Kurudisha magari
Kuhusu wajumbe kutakiwa kurudisha magari Ikulu,
taarifa hiyo imekiri ikitoa sababu kuwa kazi ya tume ilikuwa imemalizika
na kwamba magari hayo yanatakiwa kupelekwa kwenye Bunge la Katiba mjini
Dodoma.
0 comments: