Mzazi na mkazi wa Ubungo, Juma Mkopi anatamani angejaaliwa kupata watoto wa kike pekee.
Tofauti na baadhi ya wazazi wanaofikiri mtoto wa
kike hana thamani mbele ya mtoto wa kiume, yeye anatamani angekuwa na
watoto wa kike ili aidhihirishie jamii kuwa mtoto wa kike anaweza na
hata kuwa msaada mkubwa kwa familia yake na jamii kwa jumla.
Mkopi ana kisa kinachovutia kuhusu maisha yake,
kama anavyokisimulia japo kwa ufupi: “Sisi kwetu tulizaliwa wawili; dada
yangu na mimi. Niliishia kusoma A level (elimu ya sekondari kwa ngazi
ya kidato cha tano na sita), lakini dada aliendelea na kufanikiwa kufika
chuo kikuu.
“…mama yetu alikuwa muuguzi serikalini, tofauti na
baba yetu, mama alikuwa mstari wa mbele kutusimamia kuhusu elimu. Kweli
hakuwa na mchezo na elimu hasa kwa dada yangu.
Wakati mimi alikuwa ananiruhusu kwenda kucheza
mara moja moja,dada yangu ama alazimishwe kulala au awe mezani
anajisomea, niliyaona kama maisha magumu kwake, lakini leo nashuhudia
matunda yake. Hata yeye nadhani anaiona faida ya udhibiti wa mama akiwa
msichana.
“Dada amenizidi kila kitu katika maisha haya,
nitakueleza kwa nini…Unaiona hii nyumba ninayokaa? (ananyoosha kidole
kuelekea darini), siyo yangu kaniachia na familia yangu. Unadhani
imegharimu kiasi gani? Ana mengi anayofanya kwangu, kwa ndugu na
jamaa...’’
Kwa nini Mkopi anatamani angejaaliwa watoto wa
kike pekee? Anasema: “Nimejifunza kwa dada yangu namna alivyo msaada kwa
familia yetu. Uwezo wake wa fedha na hata imani ya kuwasaidia wengine,
vitu ninavyoweza kusema vimetokana na kusoma kwake, kumemwezesha
kusomesha watoto wengi katika ukoo wetu.’’
Anaongeza kusema: “Nina watoto watatu, wote wa
kiume, sitarajii kuongeza lakini ninatamani Mungu angenipatia japo mtoto
mmoja wa kike nimtengeneze kama alivyo dada yangu.’’
Ushuhuda halisi
Kisa hiki ni kielelezo madhubuti cha ukweli usio
na chembe ya shaka kuwa mwanamke ni nguzo ya jamii, ni chachu ya
maendeleo ya familia na jamii kama alivyo dada yake Mkopi. Chambilecho
msemo…ukimsomesha mwanamke, umeelimisha jamii.
Hata hivyo, ni wazazi wangapi nchini wanaotambua
ukweli huu? Kwa nini baadhi ya wazazi hawataki kuamini kuwa mtoto wa
kike akiwezeshwa anaweza kuwa kiongozi bora wa familia na jamii, au hata
kuwa msitiri wa wazazi wenyewe?
Dunia hasa ile ya kwanza inatambua nafasi na hadhi
ya mtoto wa kike, iweje sisi wa dunia ya tatu tuendelee kumdunisha
mtoto wa kike hadi kufikia hatua ya kumnyima elimu? Bado kuna mila na
desturi potofu, achilia mbali mitazamo tenge ya baadhi ya wazazi
wasioona umuhimu wa kusomesha watoto wa kike.
0 comments: