''VIONGOZI WA CCM WANAFIKI WAMEJAA CHUKI TUPU''MANSOUR

 
Siku saba tangu Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (Nec), kumvua uanachama, Mwakilishi wa Jimbo la Kiembesamaki, Mkoa wa Mjini Magharibi, Mansour Yussuf Himid, kutokana na kukiuka miiko ya chama hicho, ameibuka jana na kukiponda chama hicho kuwa kimejaa siasa za chuki na ubaguzi.
Huku akizungumza kwa umakini na kujiamini alisema, “ CCM kimejaa ubaguzi, siasa za chuki na kimeshindwa kusimamia misingi imara ya kutetea masilahi ya wananchi. Wazanzibari kataeni hali hii, wekeni tofauti za vyama pembeni, Zanzibar kwanza vyama baadaye.
Tusimamie muungano wa heshima, haki na usawa.”
Himid ambaye ni mjumbe wa Kamati ya Maridhiano Zanzibar yenye wajumbe sita, alitoa kauli hiyo jana katika kongamano la wazi lililoandaliwa na kamati hiyo katika ukumbi wa Hoteli ya Bwawani na kuongozwa na mwanasiasa mkongwe ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati hiyo, Hassan Nassor Moyo.
Katika hotuba yake ya dakika 46, Mansour ambaye kwa nyakati tofauti amewahi kuwa Waziri na Naibu Waziri wa Maji, Nishati, Ardhi na Mazingira, Waziri wa Kilimo, Waziri asiyekuwa na Wizara Maalumu na Mjumbe wa Baraza la Mapinduzi la Zanzibar, aliendelea kusimamia msimamo wa muundo wa muungano wa serikali tatu kwa kufafanua kuwa, “Muundo wa muungano wa serikali tatu ni wimbi kubwa halizuiliki tena.”
Mansour ambaye alisema hajui sababu za kufukuzwa kwake CCM, alisisitiza: “Sitakwenda mahakamani kukata rufaa kwa sababu nilichaguliwa na wananchi hivyo sitaki kuwawakilisha kwa mgongo wa mahakama,”
“Pia sina pesa za kuchezea huko mahakamani. Sihitaji malumbano, katika uchaguzi mdogo sitagombea kwa sababu sitaki kuendeleza machungu kwa wananchi wa jimbo langu na pia najiepusha na siasa za matusi, naweza kufikiria kugombea mwaka 2015.”
Katika kongamano hilo mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo, Mohamed Ahmed Al-riyami alitangaza kujivua uanachama wa CCM, kwa maelezo kuwa chama hicho kimepoteza mwelekeo
Share on Google Plus

0 comments: