''SPIKA MAKINDA ASIPUUZE USHAURI WA GAG'' MKAGUZI MKUU HESABU ZA SERIKALI (GAG)

 
Kwa mara nyingine, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ludovick Utouh amemshauri Spika wa Bunge, Anne Makinda kubadili uamuzi wake na kuzirejesha kamati za Bunge za Mashirika ya Umma (POAC) na Hesabu za Serikali (PAC), akisema ilikuwa sio sahihi kuziunganisha kamati hizo kama alivyofanya.
Kumbukumbu zinaonyesha kuwa, mapema mwaka huu, Spika Makinda aliifuta POAC na kuunganisha shughuli zake na Kamati ya PAC, hatua ambayo kiongozi huyo wa CAG anasema ilikuwa ni makosa kwa sababu uamuzi huo usingeleta ufanisi katika kutekeleza majukumu ya ofisi yake ya kudhibiti na kukagua fedha za umma. Wakati Spika Makinda alipochukua hatua hiyo, CAG huyo alionyesha wasiwasi wake hadharani na kusema ungekuwa muujiza mkubwa iwapo
hatua hiyo ya Spika ingeongeza tija na ufanisi katika ofisi yake.
Hoja ya CAG wakati huo ilikuwa kwamba shughuli za kamati hizo zilikuwa nyingi mno kiasi cha wajumbe wa kamati hizo kulemewa, kwa maana ya kushindwa kupata muda wa kutosha kufuatilia kwa umakini utekelezaji wa miradi ya maendeleo,  huduma za kijamii pamoja na kuhakiki matumizi ya fedha katika Serikali Kuu na mashirika ya umma kwa mujibu wa Ripoti ya kila mwaka ya CAG ya ukaguzi wa hesabu za taasisi hizo za umma.
Sasa baada ya miezi kadhaa tangu Spika Makinda achukue hatua hiyo, CAG amelazimika tena kutoa kauli ya kumshauri ili afikirie upya uamuzi wake wa awali. Bila shaka CAG amefikia hatua hiyo baada ya kufanya tathmini jadidi na kujiridhisha kwamba mabadiliko aliyoyafanya Spika yamedhoofisha shughuli za kudhibiti na kukagua matumizi ya fedha za umma badala ya kuongeza tija na ufanisi.
Anachosema CAG ni kuwa, hata kabla ya kamati hizo kuunganishwa, Kamati ya Mashirika ya Umma (POAC), ilikuwa tayari ikikabiliwa na changamoto kubwa ya kusimamia zaidi ya mashirika 128 ya umma nchini, hivyo hatua ya Spika kuiunganisha na Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC), ambayo ina wakala, wizara na idara mbalimbali ni kuibebesha mzigo usiobebeka.
Mengi yalisemwa wakati huo na hakika mengine mengi yameendelea kusemwa kuhusu nini hasa lilikuwa lengo la Spika katika kuchukua hatua hiyo yenye utata mkubwa.
Hadi kamati hizo zinaunganishwa, tayari zilikuwa zimejipambanua kama kamati zenye wajumbe waliokuwa wameonyesha uthubutu, uzalendo na utayari wa kupambana na ufisadi na ubadhirifu wa fedha na mali ya umma. Ni kamati zilizotumia vizuri Ripoti za CAG kupambana na uozo serikalini na mashirika ya umma na kuhakikisha hatua stahiki zinachukuliwa dhidi ya wahusika.
Hali hiyo iliwatisha viongozi serikalini na taasisi zake na mikakati ilifanyika chinichini ili kupunguza nguvu za CAG na kamati hizo. Hivyo, halikuwa jambo la kushangaza Spika Makinda alipotangaza kuunganisha kamati hizo, hatua ambayo wengi waliitafsiri kama shinikizo kutoka katika ngazi za juu serikalini.
Tunaungana na CAG, ambaye ameonyesha utumishi uliotukuka tangu ateuliwe, kumshauri Spika Makinda kutafakari upya uamuzi wake huo kwa kutenganisha kamati hizo kama ilivyokuwa awali. Sisi tunadhani kwamba uamuzi wake huo ulikuwa wa kisiasa zaidi na pengine ulilenga kuwaondoa kitanzini vigogo mafisadi walio katika utumishi wa umma.
Share on Google Plus

0 comments: