MREMA AONYA VYAMA VENYE VIKUNDI YVA ULINZI ATA HATUA ZICHUKULIWE

Mrema aonya vyama vyenye vikundi vya ulinzi
MWENYEKITI wa Chama cha Tanzania Labour (TLP), Augustine Mrema amesema kitendo cha baadhi ya vyama vya siasa kuanzisha vikundi vya kujilinda ni sawa na kudhalilisha Jeshi la Polisi. Ametaka jeshi hilo lisidhoofishwe kulinda raia, mali zao na amani ya nchi kwa kuanzisha vikundi vya kufanya kazi hiyo.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi jana, ametaka vyama na wananchi kwa ujumla, washirikiane na Serikali kuimarisha jeshi litekeleze majukumu yake.
Mrema alionya kwamba yanayotokea Misri sasa, yanaweza kutokea nchini, ikiwa hatua za pamoja za kukabili changamoto zilizopo katika jamii hazitachukuliwa kwani
ni rahisi kutengeneza vikundi vitakavyogeuka vya uasi na kuleta balaa nchini.
“Hatupaswi kukosa imani na jeshi la polisi, bado linafanya vizuri, ushahidi mzuri ni uchaguzi mdogo uliofanyika kule Arusha hivi majuzi, amani imetawala na Polisi walikuwepo kulinda, kwa nini tuanzishe vikundi vitakavyofanya kazi kama polisi?” alihoji Mrema.
Hivi karibuni, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kupitia kwa Mwenyekiti wake, Freeman Mbowe kilitangaza uamuzi wa kuanzisha kambi za mafunzo ya kulinda mikutano na viongozi wake.
Uamuzi huo wa Chadema umekosolewa siyo tu na Polisi, bali pia Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa ambaye amekionya kisithubutu kufanya hivyo akisema hatua hiyo si sahihi.
Kwa mujibu wa Tendwa, katiba ya nchi na za vyama vya siasa, hazitakuwa na maana kama kila mwananchi au kikundi wataruhusiwa kufanya mafunzo ya kijeshi au ukakamavu.
Sheria aliyoizungumzia Tendwa ni ya Vyama vya Siasa ya mwaka 1992 inayokataza chama cha siasa kushabikia, kutumika ama kutumia nguvu katika kufanikisha masuala yake ya kisiasa.
Kwa upande wa Msemaji wa Jeshi la Polisi, Advera Senso, alikaririwa hivi karibuni akisema kitendo cha chama chochote cha siasa kuanzisha kikundi cha kujihami ni kinyume na sheria za nchi akasema endapo watafanya hivyo, hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.
Alisema polisi imeanza uchunguzi na itachukua hatua kulingana na ushahidi utakaopatikana. Hata hivyo, Chadema kupitia Mkurugenzi wa Habari na Uenezi, John Mnyika, kimesema mpango wake wa kambi ya mafunzo ya kujilinda uko pale pale kwa kuwa inafanya hivyo kwa kutumia kikundi kilicho halali kwa mujibu wa Katiba mpya ya chama hicho ya mwaka 2006 ambayo Tendwa alikuwa mgeni wa heshima ilipozinduliwa.
Aidha Mnyika alisema matukio ya kushambuliwa wanachama wa chama hicho pamoja na wanataaluma wakiwemo waandishi wa habari wanaokuwa kikazi katika shughuli za chama hicho hasa mikutano ya hadhara, ndiyo msingi wa kuongeza ukakamavu kwa kundi lao la brigedia nyekundu.
Mnyika akizungumzia hilo, alisema “Kwa muda mrefu kumekuwa tukieleza kuhusu makambi ya Green Guard ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) yanayofanya mafunzo ya kijeshi…..na matukio ya kushambuliwa kwa waandishi katika mikutano mbalimbali, ushahidi wa hayo upo, nadhani afute kwanza kikundi cha CCM”.
Siku zilizopita, CCM iliwahi kueleza uwepo wa kikundi chao cha vijana cha ukakamavu kilichopo tangu zamani kwamba ni kwa ajili ya kujenga uimara wa vijana katika kukitumikia chama na nchi.
CHANZO HABARI LEO
Share on Google Plus

0 comments: