300 WATAPELIWA KUPEWA AJIRA JIJINI DODOMA

 300 watapeliwa kupatiwa ajira Dodoma
POLISI mkoani Dodoma inawashikilia watu wawili waliokuwa wakitapeli wananchi kwa kutoa vipeperushi vinavyoonesha nafasi za kazi mbalimbali za ajira kutoka kwa kampuni inayojulikana kama Granton Market Dubai (BJM).
Zaidi ya watu 300 mkoani Dodoma na mikoa mingine wanadaiwa kutapeliwa katika sakata la mlolongo wa kuahidiwa ajira; huku mmoja wao akitapeliwa Sh 400,000.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, David Misime, alisema kampuni hiyo haikusajiliwa na haitambuliki kisheria na baada ya upekuzi kufanyika katika nyumba iliyotumika kama
ofisi, zilikutwa fomu za maombi ya ajira zipatazo 320, picha ndogo za watu mbalimbali walioomba kuajiriwa.
Aliwataja wanaoshikiliwa ni Amos Magembe (25) mkazi wa Ipagala, Dodoma na Bariadi, mkoani Shinyanga. Mwingine ni Shija Stanley (27) ambaye ni mkazi wa Ipagala, Dodoma na Kiloleni, Mwanza.
Alisema uchunguzi uliofanywa na jeshi hilo uligundua kuwa kampuni hiyo haikusajiliwa na haitambuliki kisheria. Ilidai kusaka watu kwa ajili ya nafasi 92 za ajira katika maeneo tofauti kwa mshahara wa kati ya Sh 140,000 na 220,000 kulingana na kazi husika.
“Tunafanya upelelezi kubaini kama watuhumiwa hao walikuwa wakijihusisha na suala la usafirishaji haramu wa binadamu na taarifa itatolewa baadaye,” alisema.
Kamanda Misime alisema watu hao walikamatwa na Polisi kwa kushirikiana na wananchi. Walikamatwa katika mtaa wa Emmaus, Kata ya Ipagala baada ya polisi kupata taarifa kutoka kwa raia wema. Pia zilikutwa bidhaa mbalimbali zilizotengenezwa kienyeji, ikiwa ni pamoja na dawa za binadamu na manukato ya mwili.
Ilibainika kuwa ili kupata fomu ya ajira, mwombaji alipaswa kulipia Sh 4,000 kama ada ya usajili. Kamanda Misime alisema watuhumiwa wote wanatarajiwa kufikishwa mahakamani baada ya upelelezi kukamilika.
Alihadharisha wananchi juu ya watu wanaofanya utapeli kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu akisema vitendo hivyo vinaongezeka.CHANZO HABARI LEO
Share on Google Plus

0 comments: