LIGI KUU YA VODACOM KUWANIA UBINGAWA WA TANZANIA BARA MSIMU WA 2013/2014


Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kuwania ubingwa wa Tanzania Bara msimu wa 2013/2014 inaanza kutimua vumbi Agosti 24 mwaka huu kwa timu zote 14 kuwa viwanjani katika miji saba tofauti.



Hata hivyo, kabla ya ligi hiyo kuanza kutakuwa na mechi ya kufungua msimu (Ngao ya Jamii- Community Shield) kati ya bingwa mtetezi Yanga na Makamu bingwa Azam itakayochezwa Agosti 17 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.



Mechi za VPL za Agosti 14 mwaka huu zitakuwa kati ya Yanga na Ashanti United (Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam), Mtibwa Sugar na Azam (Uwanja wa Manungu, Morogoro), na JKT Oljoro na Coastal Union (Uwanja wa Kumbukumbu ya Sheikh Kaluta Amri Abeid, Arusha).



Nyingine ni Mgambo Shooting na JKT Ruvu (Uwanja wa Mkwakwani, Tanga), Rhino Rangers na Simba (Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi, Tabora), Mbeya City na Kagera Sugar (Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine, Mbeya), na Ruvu Shooting na Tanzania Prisons (Uwanja wa Mabatini, Mlandizi, Pwani).



Mzunguko wa kwanza wa ligi hiyo utamalizika Novemba 3 mwaka huu wakati wa pili utamalizika Aprili 27 mwakani.



TAIFA STARS KWENDA KAMPALA J5

Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) inaondoka Mwanza keshokutwa (Julai 24 mwaka huu) kwenda Kampala, Uganda kwa ajili ya mechi ya marudiano ya Kombe la CHAN itakayochezwa Jumamosi (Julai 27 mwaka huu) Uwanja wa Mandela kuanzia saa 10 kamili jioni.



Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager iko kambini jijini Mwanza chini ya Kocha Kim Poulsen tangu Julai 14 mwaka huu kujiandaa kwa mechi hiyo itakayoamua ni timu ipi kati ya hizo mbili itacheza Fainali za CHAN zitakazofanyika mwakani nchini Afrika Kusini.



Timu hiyo itaondoka Uwanja wa Ndege wa Mwanza saa 7.25 mchana kwa ndege ya PrecisionAir, na inatarajiwa kutua Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Entebbe saa 10.15 jioni.



Wakati huo huo, Kocha Kim Poulsen kesho (Julai 23 mwaka huu) atakuwa na mkutano na waandishi wa habari kuzungumzia maandalizi ya kikosi chake. Mkutano huo utafanyika saa 5 kamili asubuhi kwenye hoteli ya La Kairo jijini Mwanza.



WAAMUZI WA MCHEZO WA STARS VS UGANDA

Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limeteua waamuzi kutoka Madagascar kuchezesha mechi kati ya Tanzania (Taifa Stars) na Uganda (The Cranes) itakayochezwa Jumamosi (Julai 27 mwaka huu) Uwanja wa Mandela ulioko Namboole nje kidogo ya Jiji la Kampala.



Waamuzi wataongozwa na Kanoso Abdoul Ohabee wakati mwamuzi msaidizi namba moja ni Andirvoavonjy Pierre Jean Eric. Mwamuzi msaidizi namba mbili ni Jinoro Velomanana Ferdinand huku Andriamiharisoa Hubert Marie Bruno akiwa mwamuzi wa mezani (fourth official).



Kamishna wa mechi hiyo ya marudiano ya raundi ya mwisho kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN) ni Ismail Kamal kutoka Ethiopia.



Mechi hiyo namba 38 itachezwa kuanzia saa 10 kamili jioni kwa saa za Afrika Mashariki. Taifa Stars ilipoteza mechi ya kwanza iliyochezwa Julai 13 mwaka huu jijini Dar es Salaam kwa bao 1-0.



Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager iko kambini jijini Mwanza ikijiandaa kwa mechi hiyo itakayoamua ni timu ipi kati ya hizo mbili itacheza Fainali za CHAN mwakani nchini Afrika Kusini.
Share on Google Plus

0 comments: