MAMBO MUHIMU MATANO YANAYOIWEKA CCM PABAYA

Wiki mbili zilizopita Chama Cha Mapinduzi (CCM) kiliadhimisha sherehe za kutimiza miaka 37 tangua kuanzishwa, huku kikiwa na mambo matano yanayokikaba koo.

Pamoja na CCM kuendelea kuongoza nchi, ni dhahiri chama hicho kinakabiliwa na changamoto nyingi zinazoweza kusababisha kusambaratika au kung’olewa madarakani katika uchaguzi ujao wa 2015.
Dalili za kusambaratika zinatokana na mgawanyiko wa makundi, yakiwemo yale yanayonyoosheana vidole kwa ufisadi, harakati za urais 2015, hali inayoendelea ya kuumbuana hadharani huku kashfa na tuhuma za rushwa na ufisadi ndani ya chama na katika Serikali yake ziliendelea kutamalaki, mambo ambayo yanaipa picha mbaya CCM mbele ya Watanzania.
Jambo jingine ni suala la kutetea Serikali mbili ndani ya Katiba Mpya. Iwapo CCM itashindwa kutetea mfumo wa sasa wa Serikali mbili, huenda ikawa ni mwanzo wa kuonekana kuwa imeshindwa kudumisha yale yaliyoasisiwa na waasisi wa Taifa hili; Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere na Hayati, Abeid Karume.
Waasisi hao walipounganisha Zanzibar na Tanganyika na kuzaa Tanzania, waliona Serikali mbili ndizo zinazofaa kujenga mshikamano wa taifa moja, wakiamini kuwa Serikali tatu zingepanua wigo ule wa umoja.
Hata hivyo, Pius Msekwa ni mmoja wa viongozi wazoefu wastaafu ambao wametumikia chama hicho tangu mwaka 1960, anapingana na mambo hayo, akiamini kwamna CCM bado ni imara na inaendela kuungwa mkono na Watanzania walio wengi.
Kuumbuana ndani ya CCM
Pamoja na athari za wazi zinazoonekana, Msekwa anasema kauli za kuumbuana na kupakana matope zinazoendelea kujitokeza ndani ya chama hicho kuhusu urais 2015 hazina athari zozote kwa chama wala Serikali.
“Si jukumu la chama kuwanyamazisha watu, ila wasikilizaji wa kauli hizo watachambua mchele na pumba,” anasema Msekwa na kuongeza kuwa vitendo vya viongozi ndani ya CCM kunyoosheana vidole, kushutumiana na hata kudharauliana hadharani vinaashiria uhuru wa demokrasia ya maoni ndani ya chama.
Hivi karibuni Mmoja wa viongozi wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), Paul Makonda alitoa msimamo ukimtuhumu Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa kuanza kampeni za urais 2015 na kumwelezea kuwa hafai na wala hana sifa za kuwa rais.
Kauli za Makonda ziliungwa mkono na Makamu Mwenyekiti Mstaafu wa CCM, John Malecela ambaye pia alimshutumu Lowassa akidai tayari ameanza kampeni za urais kwa kusambaza fulana zinazohamasisha mtandao wa marafiki zake.
Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana kpamoja na Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nnape Nnauye, katika miezi ya karibuni waliibua suala la mawaziri saba mizigo na kuwatangaza hadharani wakimtaka Rais Jakaya Kikwete awachukulie hatua.
Share on Google Plus

0 comments: