TENGA AMKABIZI MKOBA JAMAL MALINZI KUWA RAIS MPYA WA TFF


Rais aliyemaliza muda wake Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Leodegar Tenga amemkabidhi rais mpya, Jamal Malinzi mali za TFF na amemkabidhi Sh33 milioni kwenye akaunti ya shirikisho hilo.
Akikabidhi ofisi hiyo jana, Tenga alisema fedha taslimu Shilingi 33,518,000 na Dola 1,390 zipo katika akaunti za TFF hivi sasa.
Alieleza fedha hizo zimebaki baada ya kufanya malipo ya Sh158 milioni kwa ajili ya Mkutano Mkuu na malipo ya Sh56 milioni kwa ajili matayarisho ya timu ya Taifa ya Wanawake U-20 (Tanzanite) inayokwenda Msumbiji.
“Hata hivyo, leo hii Dola 415,000 (Sh664 milioni) zimehamishwa kutoka kwenye akaunti za Kampuni ya Bia (TBL) kwenda kwenye akaunti za TFF. Fedha hizo zitakuwa tayari kwenye akaunti ya TFF ifikapo Jumanne wiki ijayo,”alisema Tenga.
Alisema, “Malipo haya yalikuwa yafanyike karibu miezi miwili iliyopita lakini yalicheleweshwa ili kutoa nafasi kwa ukaguzi wa fedha za udhamini wa TBL. Malipo mengine yanayofanana na hayo ya US $ 420,000 (Sh672 milioni) yanatarajiwa kufanyika wiki mbili kutoka sasa.”
“Ili kujiridhisha kuwa fedha za udhamini zinatumika kama ilivyokubalika katika mikataba, TFF imetoa nafasi kwa wadhamini kufanya ukaguzi wa fedha inazozitoa wakati wowote ule,” alisema Tenga.
Alisema, “Pia nakuachia Uwanja wa Karume wenye ukubwa wa ekari 8.8, hati yake ni namba 27206 ilitolewa Novemba mwaka 1981, nakuomba hati hii iwe ndiyo kitu cha kwanza kukikumbatia, naomba ukikumbatie, wasije wajanja-wajanja wakakulaghai ukaiweka dhamana,” Tenga alimwambia Malinzi.
“Kuna kiwanja kingine tumenunua Tanga mjini kina ukubwa wa ekari 19, ukarabati wa Kituo cha Ufundi umefanywa, pamoja na sababu nyingine, ili kutoa fursa kwa Mradi wa Ujenzi wa Karume kuendelea,” alisema Tenga.
Naye Rais Mpya wa TFF, Jamal Malinzi akizungumza mara baada ya makabidhiano hayo alisema, “Uchaguzi umekwisha, kama kuna ambaye tulikwaruzana kipindi cha kampeni naomba tusameheane, makundi hayajengi, tuachane nayo. Uwezo na nia tunayo, tushirikiane tufikishe soka letu mbele.
“Jumatatu ya Oktoba 28 niliahidi kuwapa ofisi vyama vya Sputanza,
Tasma, Twfa na Tafca, ofisi tayari imeshapatikana na imelipiwa mwaka mmoja maeneo ya Ilala, Cargo Stars imedhamini, baada ya msimu mmoja TFF itabidi ihangaike nayo, pia mwishoni mwa mwezi wa nne mwaka ujao, ofisi za TFF itabidi zihame hapa zilipo ili kupisha ujenzi wa mradi wa kisasa.”
Share on Google Plus

0 comments: