CATHETERIZATION LAB: MKOMBOZI ALIYETUA MUHIMBILI KUOKOA WAGONJWA WA MOYO

 
Ndoto ya Watanzania hasa wale wasio na uwezo, wanaosumbuliwa na magonjwa ya moyo kutibiwa haraka na kwa gharama nafuu inaelekea kuwa ya kweli.
Ni baada ya Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH)  kusema kuwa sasa itaweza kupunguza wagonjwa wenye matatizo ya moyo wanaokwenda kutibiwa nje ya nchi kwa asilimia 60.
Matarajio hayo ya MNH kwa wagonjwa hao yanatokana na kupata mtambo maalumu wa kisasa utakaosaidia kufanya upasuaji  wa moyo.
Mkurugenzi  Mtendaji wa MNH,Dk Marina Njelekela anasema kutokana na kupatikana kwa mtambo huo wa kisasa hospitalini hapo, wanaiomba serikali iwape fedha hasa zile ambazo imekuwa ikitumia kuwasafirisha, kuwatibu wagonjwa wa moyo hasa nchini India na kwingineko.
Badala yake, MNH inaomba fedha hizo ziwasilishwe hospitalini hapo ili wagonjwa wengi zaidi waweze kutibiwa nchini. Anasema mtambo huo unaojulikana kwa jina la Catherization Laboratory, ndiyo mtambo ambao wagonjwa wengi nchini walikuwa wakisafirishwa nje kwenda nchini India kwa ajili ya matibabu.
Anasema mtambo huo ulioigharimu serikali Sh3.6 bilioni  utasaidia katika kumchunguza mgonjwa mishipa na shinikizo ndani ya moyo na maradhi makubwa ya kazaliwa nayo kwa lengo la kujiridhisha kama anapaswa kufanyiwa upasuaji au kuwekewa kifaa saidizi katika moyo wake.
Anaongeza kuwa MNH imepata uwezo wa kupatiwa mtambo huo  baada ya baadhi ya madaktari wake kupatiwa mafunzo nchini India na Israel tangu mwaka 2008 ambapo wagonjwa 453 wenye maradhi ya moyo wamefanyiwa upasuaji.
“Kwa sasa upasuaji wa moyo unaofanyika katika hospitali  yetu (Muhimbili0  ni sawa na ule unaofanyika katika vituo vikubwa vya upasuaji moyo duniani kote,”anasema Dk Njelekela
Mkurugenzi huyo wa MNH anasema  kuwa kupatikana kwa mtambo huo kutasaidia serikali kuondokana na mzigo wa asilimia 70 ya wagonjwa wa moyo wanaopata rufaa ya kwenda kutibiwa nje.
“Sambamba na asilimia 70,  pia serikali itapunguza  gharama ya dola za Marekani 10,000 kwa kulipia matibabu ya mgonjwa mmoja anaetibiwa nje ya nchi ukilinganisha na Dola 6,000 kwa matibabu ya hapa nchini.
“Kupitia uwepo wa kituo hicho  hapa Muhimbili,  uongozi wa hospitali upo katika mazungumzo na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii ili kulipia kiasi cha dola za Marekani 6,000 badala ya dola 10,000  kwa gharama ya mgonjwa mmoja anaepatiwa rufaa ya kupeleka nje ya nchi,” anasema  Dk Njelekela .
Share on Google Plus

0 comments: