
Baada ya matokeo ya uchaguzi mkuu kutangazwa, Zimbabwe inaelekea katika
wakati mgumu wa kisiasa. Waangalizi wa SADC na Umoja wa Afrika wasema
uchaguzi umekwenda vizuri; nchi za Magharibi zakosoa hitilafu.
"Robert Mugabe achaguliwa tena kuwa rais!" Kichwa hicho cha habari
kilitawala magazeti mengi ya Kiafrika hapo jana baada ya tume ya
uchaguzi ya Zimbabwe kutangaza kuwa Mugabe amepata asilimia 61 ya kura
na hivyo kumwacha mbali kabisa mpinzani wake wa karibu Morgan Tsvangirai
wa chama cha MDC. Yeye aliambulia asilimia 34 tu ya kura.Miongoni mwa viongozi wa kwanza kumpongeza Mugabe, mwenye umri wa miaka 89, alikuwa rais wa Afrika Kusini Jacob Zuma. Alitoa pongezi zake za dhati na kuzitaka pande zote kukubali matokeo ya uchaguzi kama matakwa ya wananchi wa Zimbabwe.
Lakini kutoka nchi za Magharibi, Mugabe hakupokea pongezi. Wengi wanashuku uhalisia wa matokeo kutokana na shutuma za wizi wa kura zilizozushwa na wafuasi wa chama cha MDC na vile vile mashirika yasiyo ya kiserikali yaliyokuwa yakifuatilia maandalizi ya uchaguzi kwa karibu.
"Shutuma za wizi zichunguzwe"

Naye waziri wa mambo ya nje wa Australia, Bob Carr, ametaka uchaguzi urudiwe. Awali, waangalizi wa Jumuiya ya maendeleo ya nchi za Kusini mwa Afrika, SADC, walisema kuwa uchaguzi ulikuwa huru na wa haki. Hata hivyo, baadaye mwangalizi mkuu wa SADC na waziri wa mambo ya nje wa Tanzania, Bernard Membe, alisahihisha tamko hilo. Membe alisema: "Hatukusema kuwa uchaguzi ulikuwa wa haki. Hatukutaka kutoa tamko la mwisho haraka hivyo."
0 comments: