Mwenyekiti wa Bunge la Katiba,Samuel Sitta amekiri “kuchezewa” kwa saini ya hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere na
sehemu ya saini ya aliyekuwa Katibu wa Bunge la Tanganyika, Pius Msekwa
zilizopo kwenye hati ya sheria ya kuridhia Muungano wa Tanganyika na
Zanzibar. Akizungumza
na gazeti hili jana, Sitta alisema ni kweli kuna maneno katika hati
hiyo ya sheria namba 22 ya 1964, iliyosainiwa na Nyerere na Msekwa,
Aprili 25, 1964, yameongezwa.
Alisema
katika saini ya Nyerere kumeongezwa herufi “us” kwa kompyuta na katika
sehemu ya saini ya Msekwa kumeandikwa neno “Msekwa” kwa kompyuta, jambo
ambalo ni makosa. Sitta alisema walioongeza maneno hayo ni wafanyakazi
wa ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali baada ya kuona sehemu ya
maandishi kwenye saini hizo hayasomeki, lakini walifanya makosa.
“Wale vijana
walipoona document (nyaraka) haisomeki waliongeza “us” mwisho kwa
kompyuta kwenye saini ya Nyerere, ila walifanya makosa maana bora kitu
kionekane kufifia hivyo hivyo lakini kibaki na maana yake,” alisema.
Hata hivyo, Sitta alisema kwa waliofanya kazi na hayati Baba wa Taifa wanatambua saini iliyopo kwenye hati ya sheria hiyo ipo sawa ukiondoa makosa ya kuwekwa herufi hizo.
Kuhusu saini ya Msekwa, alisema pia kulifanyika makosa katika sehemu ya saini hiyo, kuandikwa kwa kompyuta “Msekwa”.
“Ni saini ya
Msekwa, lakini vijana wa chamber kwa AG waliongeza neno “Msekwa” kwa
kompyuta. Ni mtu asiyejua thamani na uhalisia wa saini ni kubaki ilivyo
hata kama kwa miaka 100 hata mtu aje kuisoma kwa darubini,” alisema.
Hata hivyo,
alisema maudhui ya hati ya sheria hiyo, iliyosainiwa rasmi Aprili 25,
1964 ni sahihi kama ambavyo walikubaliana waasisi wa Muungano, Nyerere
na Karume.
Alipoulizwa kuhusu suala hilo, Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema alisema kwamba hafahamu kama ofisi yake inahusika na kuchezewa kwa saini hizo, tofauti na madai ya Sitta.
Sheria iliyopitishwa Z’bar
Sitta alisema ili kuondoa utata, ameagiza kupatiwa hati ya Rais wa Kwanza wa Zanzibar, Abeid Karume (Presidential Decree) aliyotoa kusaini makubaliano kwani wakati huo, hakukuwa na Bunge.
“Karume
alitumia Baraza la Mapinduzi akatumia amri ya Rais akasaini. Tunatarajia
kuipata hiyo, sasa tutakuwa tumepata nyaraka za Bara na Zanzibar,”
alisema Sitta.
Hata hivyo, alisema kisheria kilichopitishwa na Bunge la Tanganyika na Baraza la MapinduziZanzibar ni yaleyale yaliyopo kwenye mkataba wa Muungano.
“Unajua
kuhoji sasa mambo haya ni kupoteza muda, ni kama kuulizana na mke wako
cheti cha ndoa baada ya kuishi pamoja miaka mingi, jana (juzi) nilikuwa
nawaomba wajumbe kujua tunachotakiwa ni kutengeneza Katiba ambayo,
inajibu matatizo yetu,” alisema Sitta.
Hati ipo UN - Akizungumzia
hati ya Muungano, alisema kuwa ni kweli kupata hati hiyo kuna umuhimu,
lakini mambo yote muhimu yanayohusu Muungano yamewekwa katika sheria
hizo mbili zilizoridhiwa na pande zote.
Alisema kwa
muda walionao wajumbe wa bunge hilo, lazima wautumie vizuri kuliko
kwenda hadi Umoja wa Mataifa (UN) kwa ajili ya kuchukua hati hizo.
“Bunge la
Tanganyika lililetewa muswada unaoonyesha mambo waliyokubaliana Nyerere
na Karume, na Baraza la Mapinduzi likapelekewa hivyohivyo,” alisema na
kuongeza: “Sasa ubishi wa hiyo hati ya kwanza kabisa ambayo wengi
wanasema ipo Umoja wa Mataifa ilikopelekwa kuthibitisha nchi imebadili
jina, hiyo ni ya nini? Ni ubishi wa bure tu.”
Sitta
alisema kisheria kilichopitishwa na Bunge kinatambua yaliyomo katika
hati hiyo na hali ndivyo ilivyo pia kwa Baraza la Mapinduzi.
Kwa takriban siku tatu,
kamati kadhaa za Bunge zinazojadili Rasimu ya Katiba, zimekuwa na
mgongano juu ya hati za muungano na uhalali wa saini za Nyerere na
Msekwa.
Kanuni kutenguliwa - Alisema pia, Bunge la Katiba itabidi kubadili kanuni na ratiba yake katika kikao cha leo.
Sitta
alisema kwa utaratibu uliokuwapo, leo kamati ndio zilipaswa kuanza
kuwasilisha taarifa zake, lakini imeonekana haiwezekani.
“Ni kamati
moja tu Namba 5, kati ya kamati 12 ndio ambayo ilikuwa imekamilisha
kujadili na kupiga kura walau Sura ya Kwanza tu ya Rasimu, hivyo kwa
hali ilivyo lazima tupitie upya kanuni zetu,” alisema Sitta.
“Tuliweka
siku moja kwa ajili ya uandishi na kuandika ripoti, lakini haiwezekani,
imebidi tuongeze siku nyingine moja ili wajumbe waweze kuipitia tena
taarifa ya kamati ambayo itasomwa bungeni, vinginevyo itasababisha
ubishi,” alisema.
Alisema marekebisho yote ya kanuni, yatafanyika leo bungeni na baadaye ndio itatolewa Ratiba ya Bunge katika siku zijazo.
Hata hivyo,
alisema katika ratiba hiyo, kutakuwa na mapumziko ya Bunge Aprili 7,
kupisha maadhimisho ya Siku ya Karume, baadaye Ijumaa Kuu, Sherehe za
Pasaka na pia maadhimisho ya Sokoine na Muungano.
Chanzo - Mwananchi
0 comments: