DIMBA NA CHAN ZAINGIA NUSU FAINALI

Katika dimba la Kombe la Mataifa ya Afrika kwa wachezaji wa timu za nyumbani, CHAN, Ghana, Libya, Nigeria na Zimbabwe zimeingia katika awamu ya nusu fainali mwishoni mwa wiki.
Ghana ilifunga Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo goli moja kwa sifuri katika mechi ya mwisho ya robo fainali, na hivyo kujikatia tikiti ya kucheza mechi ya utani wa jadi dhidi ya mahasimu wake Nigeria katika nusu fainali. Kwabina Adusei alisukuma wavuni mkwaju wa penalty katika dakika ya 67.
Mapema jana jioni Libya iliipiku Gabon kwa mikwaju ya penalty katika mpambano mkali kabisa ambao ulikamilika kwa sare ya goli moja kwa moja katika muda wa kawaida na wa ziada. Sasa Libya itatiana kifua na Zimbabwe katika nusu fainali.
Siku ya Jumamosi, Nigeria ilinusia kichapo lakini ikapata ushindi wa magoli manne kwa matatu baada ya mechi kuingia muda wa ziada dhidi ya Morocco. Zimbabwe nayo iliwashangaza waliopigiwa upatu Mali kwa kuwafunga mabao mawili kwa moja. Mechi zote za nusu fainali zitachezwa Jumatano wiki hii.
Mwadishi: Bruce Amani/AFP/DPA
Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman
Share on Google Plus

0 comments: