''VIJANA HACHENI KUKIMBILIA SAUZI SIO PEPONI'' BALOZI MSUYA


Kwa siku za karibuni limetokea wimbi kubwa la vijana  wa Kitanzania kukimbilia nchi mbalimbali duniani ikiwamo Afrika Kusini kwa madai ya kusaka maisha bora.
Baadhi ya vijana hao wamekuwa wakikamatwa na hata kurudishwa nchini baada ya kukosa uhalali kisheria wa kuendelea kuishi katika nchi hizo.
Wengine kati yao wamejikuta matatani kwa kuhusishwa na usafirishaji wa dawa za kulevya pamoja na maovu mengine baada ya  kuingia katika nchi hizo kwa njia halali na zisizo halali.
Kwa upande wa Afrika Kusini, baadhi ya vijana hao wemeamua kuhamishia shughuli zao za kibiashara nchini humo.
Balozi wa Tanzania nchini humo, Radhia Msuya  anasema vijana wengi wanadanganyika kwa kufikiri kuwa maisha katika nchi hiyo ni rahisi na kuwa baada ya kufika huko mambo yatakuwa rahisi na kinyume chake mambo huwawia magumu na baadhi yao kuhitaji msaada wa kurudishwa nyumbani.
Vijana 200 kwa mwezi
Balozi Msuya anasema kila mwezi wastani wa vijana  200 hurudishwa nyumbani Tanzania kutoka nchini humo kutokana na sababu mbalimbali wakiwamo wale walioingia katika nchi hiyo bila vibali.
 ‘’Huku siyo peponi, maisha bora yanafanyiwa kazi kama ilivyo huko nyumbani. Kila mwezi tunarudisha nyumbani vijana  200 wanaokamatwa mitaani hapa wakiuza  bidhaa ndogo ndogo huku wengi wao wakiwa hawana vibali,’’ anasema Balozi Msuya.
 Anasema shughuli ndogo ndogo za biashara wanazofanya vijana hao kutoka Tanzania haziwawezeshi kumudu gharama kubwa za maisha nchini humo na baadhi yao hudaiwa kujihusisha na vitendo vya uhalifu, ikiwemo matumizi ya dawa za kulevya.
Aidha, balozi  huyo  anawataka vijana wasiamini kuwa majibu yote ya changamoto zote zinazowakabili yanapatikana serikalini.
Anasema  baadhi ya majibu ya changamoto hizo yako mikononi mwao na utatuzi wake siyo lazima kukimbilia nchini humo.
 Anasema ni kweli  Afrika Kusini imepiga hatua kubwa kimaendeleo katika sekta mbalimbali ikiwamo maendeleo  ya kiuchumi, ingawa  pia yapo matatizo mengi  ambayo vijana hukumbana nayo baada ya kufikiri kwamba kukimbilia nchini humo litakuwa ni suluhisho la matatizo yote waliyoacha nyumbani.
Share on Google Plus

0 comments: