Marekani na Urusi Jumamosi (14.09.2013) zimefikia makubaliano ya
kihistoria baada ya mazungumzo ya siku tatu juu ya mpango mkubwa wa
kutokomeza silaha za sumu za Syria kufikia kati kati ya mwaka ujao wa
2014.
Waziri wa mambo ya nje wa Marekani John Kerry na mwenzake wa Urusi Sergei Lavrov wakiwa Geneva. (14.09.2013).
Kulingana na makubaliano hayo mataifa hayo mawili yenye nguvu duniani
yamempa Rais Bashar al Assad wa Syria wiki moja kuwasilisha maelezo juu
ya silaha za sumu zilizolimbikizwa na utawala wake.Waziri wa mambo ya nje wa Marekani John Kerry amesema utawala wa Assad lazima utowe nafasi mara moja kwa wakaguzi kutoka Shirika Lenye Kupiga Marufuku Silaha za Sumu (OPCM) kuziona silaha hizo.
Kerry ameuambia mkutano wa waandishi wa habari wa pamoja na waziri mwenzake wa Urusi Sergei Lavrov kwamba wakaguzi hao wanapaswa kuwa huko kabla ya mwezi wa Novemba na lengo ni kuanza kuondowa silaha hizo kuelekea mwakani.
Akirudia onyo kutoka kwa Rais Barack Obama kwamba hatua za kijeshi zitachukuliwa na Marekani na washirika wake iwapo diplomasia itashindwa kufanya kazi ,Kerry ameonya kwamba hakupaswi "kuwepo mchezo na chochote kile ziada ya utawala wa Assad kutii kikamilifu uwondoaji wa silaha hizo."
Makubaliano kujumuishwa kwenye azimio la Umoja Mataifa
Waziri wa mambo ya nje wa Marekani John Kerry na mwenzake wa Urusi Sergei Lavrov wakipongezana mjini Geneva. (14.09.2013).
Kerry amesema hatua zilizokubaliwa Jumamosi zitajumuishwa
katika azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa
litakalotayarishwa chini ya kifungu nambari saba cha katiba ya umoja huo
ambacho kinazungumzia uwekaji wa vikwazo na uwezekano wa matumizi ya
nguvu za kijeshi.Lakini kutokana na Urusi kupinga vikali vitisho vya matumizi ya kijeshi na ikiwa na uwezo wa kura ya turufu katika Baraza la Usalama,Kerry amekiri kwamba ilikuwa haiwezekani kufikiwa makubaliano ya mapema juu ya kile kitakachotokea iwapo Syria itashindwa kutii azimio hilo.
Lavrov amedokeza kwamba serikali ya Urusi itaunga mkono aina fulani ya vikwazo kwa kusema kwamba Baraza la Usalama litachukuwa hatua chini ya Kifungu nambari Saba iwapo Syria itashindwa kutimiza masharti yake.
Suluhisho ni diplomasia
Waziri wa mambo ya nje wa Marekani John Kerry akizungumza katika mkutano wa waandishi wa habari mjini Geneva.(14.09.2013).
Kerry amesema vita vya maafa vya wenyewe kwa wenyewe nchini
Syria ambayo vimesababisha zaidi ya vifo 110,000 katika kipindi cha
miaka miwili na nusu vitaweza tu kukomeshwa kwa kupitia mazungumzo.Huo unaonekana kuwa ni uungaji mkono mwengine kwa upinzani wa Urusi kwa aina yoyote ya uingiliaji kati kijeshi na unaweza kutafsiriwa kama Marekani inaachana na msimamo wake kuwapatia msaada waasi kuwasaidia kumn'gowa madarakani Assad.
Kerry amekaririwa akisema " hakuna ufumbuzi wa kijeshi kwa mzozo nchini Syria na unabidi uwe wa kidiplomasia na tunahidi kuendelea kuishirikiana kufanikisha hilo."
Lavrov ameyapongeza makubaliano hayo kama ni makubaliano mazuri kabisa ambapo umuhimu wake ni vigumu kukadiria kupindukia.
Upinzani wayakataa makubaliano
Generali Selim Idriss mkuu wa Jeshi Huru la Syria.
Makubaliano hayo yamepokelewa kwa fadhaa na muungano wa
upinzani wa Syria ambao umetumia miaka miwili kuyaomba mataifa ya
magharibi kuwapatia silaha wanazohitaji kuupa nguvu katika vita hivyo
vya wenyewe kwa wenyewe.Generali Selim Idriss mkuu wa Jeshi Huru la
Syria amewaambia waandishi wa habari mjini Istanbul kwamba"Hawawezi
kukubali sehemu yoyote ile ya mpango huo."Amesema inamaanisha kwamba "Wao Wasyria wanatakiwa wasubiri hadi kati kati ya mwaka 2014, waendelee kuuwawa kila siku na kukubali makubaliano hayo kwa sababu tu silaha za sumu zitaangamizwa hapo mwaka 2014."
Mapambano nchini Syria kwenyewe yanazidi kupamba moto ambapo waasi na vikosi vya serikali wako katika mapigano makali ya kutaka kuudhibiti mji wa kale wa Kikrito wa Maalula ulioko karibu na Damascus.
Matumaini kufufua mazungumzo ya amani
Waziri wa mambo ya nje wa Urusi Sergei Lavrov akizungumza katika mkutano wa waandishi wa habari mjini Geneva.(14.09.2013).
Serikali ya Marekani na Urusi zinataraji kufufuwa mipango ya
mazungumzo ya amani huko Geneva ambayo yataukutanisha utawala wa Assad
na upinzani katika kufikia makubaliano juu ya kipindi cha mpito cha
kisiasa kukomesha vita hivyo ambavyo vimezuka hapo mwezi wa Machi mwaka
2011.Kerry na Lavrov watakutana tena wiki chache zijazo pembezoni mwa mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mjini New York kwa matumaini ya kupanga tarehe ya mkutano huo wa amani uliokwama.
Tangazo la ghafla la Urusi kwamba Syria iko tayari kukabidhi silaha zake za sumu limemfanya Obama kusitisha mashambulizi ya kijeshi ambayo Marekani na Ufaransa yalitishia kufanya dhidi ya Syria kutokana na shambulio la silaha za sumu lililofanyika hapo mwezi wa Augusti karibu na Damascus ambalo Marekani inaulaumu utawala wa Syria kwa kuhusika nalo na kusema limeuwa takriban watu 1,400.
Mwandishi: Mohamed Dahman/AFP
0 comments: