OBAMA AFUTA ZIARA ZAKE ZA KUTEMBELEA MBUGA ZA WANYA YADAIWA NI KUTOKANA NA VURUGU ZA KISIASA ZILIZOTOKEA MKOANI ARUSHA NDIO ZIMESABABISHA


MADHARA ya vurugu za kisiasa mkoani Arusha zinazodaiwa kusababishwa na polisi kukabiliana na wafuasi wa vyama vya upinzani, zimesababisha pigo kubwa kiuchumi katika ziara ya Rais wa Marekani, Barack Obama, Tanzania Daima Jumapili limebaini.
Pigo hilo ambalo limesababisha serikali na mahoteli ya kitalii mkoani humo kukosa mabilioni ya fedha, limetokana na hatua ya rais huyo na ujumbe wake kufuta ziara yake kwenye mbunga za wanyama za Serengeti na Mikumi.
Hatua hiyo imeelezwa kuwa ni pigo kwa serikali ambayo ilitarajia kuingiza mabilioni ya fedha baada ya rais huyo maarufu duniani na ujumbe wake wa watu 700, kuzuru kwenye hifadhi hizo za taifa.
Rais Obama ambaye alianza ziara yake barani Afrika nchini
Senegal, alipata fursa ya kutembelea sehemu za utalii na hata alipokuwa nchini Afrika Kusini, alitembelea sehemu ya utalii, hususan gereza alilopata kufungwa Rais wa kwanza mweusi wa nchi hiyo, mzee Nelson Mandela, ambaye kwa sasa yu mahututi.
Habari kutoka ndani ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa zilisema Rais Obama ambaye anatarajiwa kuwasili kesho nchini, akitokea nchini Afrika Kusini, amefuta ziara hizo kwa sababu za kiusalama, hususan hali tete iliyoko mkoani Arusha.
Kwa mujibu wa habari hizo, hali tete ya Arusha, imesababisha mikutano mingine mikubwa ya kimataifa kufanyika jijini Dar es Salaam.
Jiji la Dar es Salaam linatarajiwa kuwa na wageni 2,700, wakiwamo wajumbe 800 kutoka nchi mbalimbali duniani, wanaohudhuria mkutano wa Majadiliano ya Kimataifa kwa Manufaa ya Wote (ISPD), 2013. Mkutano huo unafanyika katika ukumbi mpya wa kisasa wa Mwalimu Nyerere. Umewahusisha marais tisa, marais wastaafu watano na wakuu wa serikali.
Mbali ya ujio wa Rais Obama na ujumbe wake wa watu 700, serikali pia inatarajia kupokea wajumbe wengine wa mkutano wa wake za marais barani Afrika. Mikutano yote hiyo itafanyika jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya maofisa wa wizara hiyo ambao waliomba majina yao yahifadhiwe, waliliambia gazeti hili kuwa, katika hali ya kawaida mikutano hiyo ingefanyika mjini Arusha ambako kuna hali ya hewa ya baridi inayofanana sana na maeneo waliyotoka wageni wengi.
Wameeleza kuwa mandhari na ufinyu wa Jiji la Dar es Salaam kumeifanya serikali mara nyingi kufanya mikutano mikubwa ya kimataifa jijini Arusha ambako pia kuna hifadhi za utalii.
“Haya ni madhara ya kucheza na amani, hatutaki kunyoshea kidole mtu yeyote, lakini sote tunahusika katika hali hiyo. Tunaweza kuilaumu serikali, polisi na vyama vya siasa, lakini ni sote,” alisema mmoja wa viongozi wa wizara hiyo.
Akizungumzia kufutwa kwa ziara ya Rais Obama kwenye hifadhi za taifa, Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki, alisema Rais Obama hakuwa na mpango wa kwenda Serengeti bali alitaka kwenda Mikumi.
“Ni kweli amefuta ziara ya kwenda Mikumi, lakini hakuwa na mpango wa kwenda Serengeti na si kwa sababu za kiusalama,” alisema Waziri Kagasheki.
Matukio makubwa ya milipuko ya mabomu iliyotokea hivi karibuni mkoani Arusha, moja katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi Parokia ya Olasikiti na jingine kwenye mkutano wa hadhara wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), huku polisi ikishindwa kuwanasa watuhumiwa, yameitia doa serikali ya Rais Jakaya Kikwete.
Katika mlipuko wa bomu la hivi karibuni katika mkutano wa hadhara wa CHADEMA, zaidi ya watu wanne wamepoteza maisha huku mawaziri wa serikali wakionekana dhahiri kuinyoshea kidole CHADEMA, huku CHADEMA wakiinyoshea kidole serikali na Chama chake Cha Mapinduzi (CCM) kwamba wanahusika.
Kishindo cha ujio wake kesho
Ukiachia kasoro hiyo, maandalizi ya ujio wa rais huyo yamekamilika.
Rais Obama, anatarajiwa kutua kesho saa 8:40 mchana, huku maofisa wa Marekani wakilazimika kushika majukumu yote katika uwanja huo, ikiwamo kuongoza ndege, ukaguzi wa abiria na mizigo.
Kazi ya kuongoza ndege ambayo kwa kawaida hufanywa na Mamlaka ya Anga Tanzania (TAA), kesho kazi hiyo itasimamiwa na Wamarekani wenyewe.
Hata idadi ya maofisa wa Tanzania wakiwamo viongozi watakaompokea Rais Obama siku hiyo pia itapangwa na Wamarekani wenyewe.
Wakati huduma ya zimamoto ikiwa inahitajika zaidi wakati ndege inapotua au kupaa, maofisa wa usalama wa Marekani wamekataa kutumia zimamoto wa Tanzania.
Tayari magari 150 ya msafara wa ziara yake yamewasili nchini, huku serikali kwa kushirikiana na makachero wa Marekani wakifanya mchujo wa majina machache ya mawaziri watakaoruhusiwa kumpokea kiongozi huyo maarufu zaidi duniani.
Mkurugenzi wa Uwanja wa Ndege wa Mwalimu Julius Nyerere, Moses Malaki, aliliambia gazeti hili jana kuwa matayarisho ya ujio wa rais huyo hayajapata kutokea nchini.
Tanzania Daima Jumapili ambayo jana ilikuwa ikipita katika maeneo mbalimbali ambayo Rais huyo atapita, imeshuhudia kuwapo kwa ukaguzi wa hali ya juu ukifanywa na makachero wa Marekani katika kuimarisha ulinzi.
Wamarekani wameamua kufanya kila kitu wenyewe, kwa kuwa hawamwamini mtu yeyote, wakiwamo maofisa usalama wa Tanzania.
“Mazoezi haya yatatoa picha rasmi ya jinsi rais huyo atakavyotua, wapi bendi ikae, wapi maofisa wasimame, wapokeaji na msafara wake mzima,” alisema.
Kinachoendelea ndani ya Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere ni mazoezi ya kumpokea Rais Obama, hususan jinsi watu wanavyotakiwa kujipanga.
Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, alisema wakati huu wa ujio wa Obama ulinzi ni mkali na wa kutisha kwa wahalifu.
Alisema mtandao mkubwa wa askari umeshawekwa tayari barabarani kuhakikisha kila kitu kinakwenda kama ilivyopangwa hadi siku ya tukio lenyewe ambayo ni kesho.
Share on Google Plus

0 comments: