Sisi hatuna
ugomvi na agizo hilo la Rais ambalo tunadhani alilitoa kwa nia njema tu.
Tukitilia maanani maisha ya taabu yanayowasibu wananchi wanaohamishwa
kutoka sehemu wanazoishi ili kupisha miradi ya Serikali, tutagundua
kwamba fidia zinazotolewa kwa wananchi hao ni kidogo mno na hakika
haziwezi kukidhi gharama za maisha mapya kwa wananchi hao, zikiwamo za
ujenzi wa makazi.
Wasiwasi
wetu unakuja pale tunaposhindwa kuelewa vigezo alivyotumia kuona kwamba
wananchi watakaohamishwa kupisha ujenzi wa bandari hiyo wanastahili
kujengewa nyumba, wakati wananchi wengi wilayani Bagamoyo tayari
wamechukuliwa ardhi yao kupisha miradi ya uwekezaji inayosimamiwa na
EPZA kwa niaba ya Serikali. Jambo la ajabu ni kwamba wengi wa wananchi
hao sio tu kwamba hawakujengewa nyumba, pia hawajalipwa fidia hata senti
moja tangu ardhi yao ichukuliwe na Serikali miaka mitano iliyopita.
Hapa
tunazungumzia wananchi wa vitongoji vya Gongoni, Kibuba, Mchanga wa
Kichwa, Changuruwe, Mkungarungo na vingine kadhaa katika Kijiji cha
Zinga. Hapa hatujataja vitongoji vingine nje ya kijiji hicho kama
Kiromo, Pande, Makondo na kadhalika. Zipo fununu kwamba wananchi
waliolipwa ni wale walio katika vitongoji ambavyo baadhi ya wamiliki wa
ardhi ni vigogo wenye ukwasi na ushawishi mkubwa serikalini.
Tunachotaka
kusema hapa ni kwamba tunadhani Rais Kikwete hajui kuwapo kwa hali hiyo.
Kwa jinsi tunavyomfahamu, angejua hali hiyo angemwagiza kiongozi huyo
wa EPZA na wizara husika ziwalipe wananchi hao fidia haraka
iwezekanavyo. Hoja yetu hapa ni kwamba Rais angehimiza utekelezaji wa
Sheria ya Ardhi ya Vijiji ya 1999 (Na 4 & 5 ya 1999) chini ya Kanuni
ya 6 kuhusu madai ya fidia ya ardhi ya mwaka 2001.
Ni kashfa na
aibu kubwa kwa Serikali kuwadhulumu wananchi wake mchana kweupe, tena
kinyume na sheria hiyo ya Ardhi tuliyoinukuu hapo juu. Wananchi hao
wamekuwa wakiahidiwa fidia tangu mwaka 2009. Sasa wanateseka, wanalia na
kusaga meno. Hawana pa kusemea, ingawa sasa wanajipanga kwenda
mahakamani. Ardhi hiyo sasa imepanda thamani kiasi cha kutisha, lakini
siyo yao tena. Walikuwa wakiitegemea kwa kila kitu. Upole wao na utiifu
wa sheria umewaponza, kwa maana kwamba pengine wangeandamana na kufanya
vurugu kama tunavyoshuhudia wengine wakifanya katika sehemu kadhaa
nchini, huenda Serikali ingekuwa imewalipa fidia ya ardhi yao.
Tunamshauri
Rais Kikwete aingilie kati suala hilo la fidia kwa wananchi hao.
Inaonekana kwamba wizara husika za Fedha, Biashara na Viwanda, Ardhi
pamoja na ile ya Uwekezaji hazina ushirikiano na pengine ndiyo sababu
hazina habari na kinachoendelea. Hivi tujiulize, Serikali inapata faida
gani inapotengeneza mazingira ya wananchi kuwa na chuki dhidi yake?
Chanzo - Mwananchi
0 comments: